Elimu ya kilimo cha tija yawafikia wakulima wa mikoa mitano.
Na Israel Mwaisaka,Rukwa
MRADI wa Kilimo na Lishe Tanzania (NOURISH -Tanzania), umelenga kuwafikia wakulima 168,000 katika mikoa mitano nchini kwa lengo la kuwaelimisha kuhusu kilimo cha tija ili iondokane na umaskini pia kuleta mapinduzi kwenye sekta hiyo.
Elimu hiyo imejikita katika kuelimisha wakulima hao kuhusu usalama wa chakula, lishe bora, kilimo kinachohimili mabadiliko ya tabia nchi na mbegu bora.
Akizungumza kwa nyakati tofauti katika vijiji vya kijiji Matai Asilia na Mkowe katika Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo mkoani Rukwa , Ofisa wa Mradi wa NOURISH, Fikilio Gambi amesema tangu mradi huo uanze mwaka jana umewafikia wakulima 13,556 katika mikoa ya Rukwa na Songwe kwa kutoa elimu kwa wakulima hao ambao ni wanufaika wa mradi pamoja na jamii nzima ili kuleta mapinduzi makubwa katika sekta ya kilimo.
Alisema wakulima hao wamefundishwa elimu ya lishe,kilimo chenye tija, usafi binafsi na usafi wa mazingira pamoja na kushiriki katika miradi mbalimbali ambayo itawasaidia kuongeza kipato.
Alisema mradi huo unafadhiliwa na Shirika la Maendeleo Norway (Norad) na kutekelezwa na wadau wa maendeleo SNV pamoja na Farm Africa kupitia washirika wake RECODA na MIICO.
Gambi alisema mikoa mitano itakazonufaika na elimu hiyo ni pamoja na Dodoma, Manyara, Rukwa, Singida na Songwe.
Alisema sambamba na hayo wakulima hao watapata fursa ya kujifunza moja kwa moja kutoka kwenye mashamba ya mfano yaliyofanikiwa, kuunganishwa na biashara za kilimo.
Akizungumzia mafanikio ya mradi huo kwa kipindi cha mwaka mmoja uliopita Gambi alisema: “Mradi wa NOURISH wilayani Kalambo umefanikiwa kuelimisha juu ya wananchi jinsi ya kuanzisha mashamba darasa 195 kwa mazao ya mtama,maharagwe na alizeti kwa kuzingatia kanuni bora za kilimo pia kuwaunganisha wakulima na kampuni za pembejeo bora za kilimo (mbegu na viatilifu )" anasema Gambi
Anaongeza kuwa mradi ho umeanzisha 130 vikundi vya kilimo pia kupitia mradi juo wakulima wamepewa pembejeo za kilimo kwenye mashamba darasa na kugawa kilogramu za mbolea ya kupandia na mbolea ya kukuzia kilogramu 2,458, mbegu bora kilo 760,viatilifu lita 130 na viuakuvu kilo 65.
Ofisa Kilimo Wilaya ya Kalambo,Jonathan Leza amewataka wakulima washiriki wa mradi huo kuwa chachu ya maendeleo na watekeleza kwa vitendo kwenye kaya zao yale waliyofundishwa lakini pia kushirikishe wanavikundi wengine elimu hiyo.
Katika mikoa hiyo mitano Mradi wa NOURISH kwa mwaka mmoja umeleta mafanikio makubwa kwa wakulima zaidi ya 6,000 wameunganishwa na wasambazaji wa pembejeo, watoa huduma 472 wa afya ya jamii wamefundishwa kuhusu lishe bora, na zaidi ya wakulima viongozi 400 wamepata mafunzo ya kilimo kinachozingatia mabadiliko ya tabianchi .



Comments
Post a Comment