WAANDIKISHAJI WAPIGA KURA WATAKIWA KUFANYA KAZI YAO KWA UWELEDI ILI KUFANIKISHA JUKUMU HILO LA KITAIFA




Na Israel Mwaisaka,Nkasi

WASHIRIKI wa mafunzo ya uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura awamu ya pili wametakiwa kufanya kazi yao kwa ueledi mkubwa ili kuweza kufanikisha jukumu hilo la msingi la kitaifa na kuhakikisha wale wote wenye sifa wanajiandikisha katika daftari hilo.
Wito huo umetolewa jana na afisa mwandikishaji  wa wilaya Nkasi  Ladislaus Mzelela  alipokuwa akifunga mafunzo ya  siku moja  kwa maafisa Waandikishaji wasaidizi na waendesha vifaa  ambapo amedai kuwa jukumu lao ni kubwa hivyo uweledi pekee utapelekea kufanikisha kazi hiyo kwa ufanisi.




Alisema kuwa mafunzo hayo  waliyoyapata kwa njia ya nadharia na vitendo yalijikita katika ujazaji fomu mbalimbali zitakazotumika vituoni  fomu za kiapo cha kutunza siri na kujitoa uanachama katika chama cha siasa ikiwa ni pamoja na namna ya kuandikisha wapiga kura wapya,wanaorekebisha au kuboresha taarifa zao ikiwa ni pamoja na wale wanaoondolewa au kufutwa kwenye daftari la kudumu la mpiga kura.

Hivyo amewataka kutambua  uzito na umuhimu wa zoezi hilo la kitaifa na kwa kuwa wameelewa mafunzo hayo kwa kina hivyo elimu na ujuzi walioupata ikawasaidie kutekeleza jukumu hilo la msingi katika kuhakikisha wale wote wenye sifa stahiki wanapata nafasi ya kuandikishwa katika daftari la kudumu la mpiga kura.




Mzelela  amewataka waandikishaji hao kutambua kuwa wanalo jukumu na madaraka makubwa katika vituo vyao vya kuandikisha  na kuwa kazi ikienda mrama uadilifu wao utatiliwa mashaka na athari zake zitatikisa taifa.

Pia amewataka Wananchi kujitokeza kwenda kujiandikisha kwenye daftari hilo kuanzia Mei 1,2025  zoezi ambalo litadumu kwa muda wa siku saba.

afisa uchaguzi wilaya Nkasi Atufigwege Mwakitega kwa upande wake aliwataka  maofisa hao waandikishaji kuhakikisha wanavitunza vyema   vifaa watakavyokabidhiwa kwa ajiri ya kazi hiyo na kuwa kazi hiyo ili iweze kuleta tija inategemea vifaa hivyo kwa maana hiyo kuna sababu za kuvitunza vifaa hivyop kwa umakini mkubwa.

Na aliwataka waandikishaji katika vituo watakavyopelekwa kuhakikisha kwamba wanakua na tabia njema na busara kitu ambacho kitahakisi kazi njema waliyotumwa na tume huru ya taifa ya uchaguzi na kuwaomba kutojihusisha na vitendo vya ulevi katika kipindi chote cha siku 7 watakapokuwa wakitekeleza jukumu hilo kubwa na la msingi.



Washiriki wa mafunzo hayo waliahidi kwenda kuifanya kazi hiyo kwa weredi mkubwa na kuwa kila walichojifunza watakifanya kwa vitendo ili kila mmoja mwenye haki ya kuandikishwa anaandikishwa kwa mujibu wa sheria

Mwisho

Comments

Popular posts from this blog

KAEGELE NA KAZUKAMWE WAIBUKA KIDEDEA KURA ZA MAONI CCM WILAYANI NKASI

DIWANI KATA YA KALA AFARIKI DUNIA KWA UGONJWA WA KIHARUSI

Mke wa Mchungaji wa kanisa la EAGT ajinyonga akihofia deni lake la fedha za kanisa