Watakiwa kujitokeza kupiga kura uchaguzi mdogo ili kutimiza haki yao ya kikatiba
Na Israel Mwaisaka,Sumbawanga
MWENYEKITI wa tume ya taifa ya Uchaguzi taifa ,jaji wa Mahakama ya Rufaa Jacobs Mwambegele amewataka wananchi wa kata ya Kabwe wilayani Nkasi mkoani Rukwa kujitokeza kupiga kura kwenye uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata hiyo ili kuweza kutimiza haki yao ya kidemokrasia.
Akizungumza jana katika ofisi ya mkurugenzi mtendaji wa wilaya amesema kuwa uchaguzi huo unatarajia kufanyika Marchi 20 na uchaguzi huo utafanyika katika kata 23 za Tanzania bara.
Amesema kuwa kwa kata ya Kabwe vyama sita vya siasa vimejitokeza kusimamisha Wagombea ambavyo ni NCCR-Mageuzi,ADA Tadea,CCM,ACT-Wazalendo,CHAUMA na chama cha UDP
Jaji Mwambegele amedai kuwa karibia maeneo yote kutakakofanyika uchaguzi huo mdogo kila kitu kinaenda vizuri na kuwa kwa sasa vyama vyote vya siasa vinaendelea na kampeni ya kunadi sera zao.
Hivyo amevitaka vyama vya siasa kuendelea na mchakato wa kampeni za kisiasa vizuri kwa kufuata kanuni na sheria huku akiwatoa wasiwasi wananchi ya kuwa atakayeshinda kwenye uchaguzi ndiye atakayetangazwa na kuwa jukumu la kumtangaza mshindi ni la tume ya uchaguzi na si vinginevyo.
Uchaguzi mdogo katika kata ya Kabwe unatokana na diwani aliyekuwepo Ahsante Lubisha (CHADEMA) kufariki dunia kutokana na ajali ya gari aliyokuwa akiiendesha yeye mwenyewe


Comments
Post a Comment