Serikali yachanja mbuga, uwekezaji bandari Jumatatu, Agosti 28, 2023
Dar es Salaam.
Serikali imesema inaandaa nyaraka kwa ajili ya utekelezaji wa makubaliano ya uwekezaji wa bandari kati yake na Dubai.
Hatua hiyo inakuja wakati bado kukiwa na ukinzani wa maoni, kuhusu makubaliano hayo kutoka kwa makundi mbalimbali nchini.
Akijibu maswali ya waandishi wa habari katika mkutano Jumamosi Agosti 26, 2023, Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa alieleza hatua hiyo inafuata baada ya Serikali kushinda kesi hivi karibuni.
“Hakuna ukimya, Serikali ilishasema kwamba inapokea maoni ya Watanzania, baada ya kukamilisha michakato yote. Bunge limeridhia, hatua inayofuata sasa ni kuandaa nyaraka. Zikikamilika ndiyo tunakwenda kuandaa miradi ya utekelezaji,” alisema Msigwa alipojibu swali la John Marwa wa Jambo TV.
“Kinachofanyika ni hivi; baada ya makubaliano kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Dubai ni mikataba ya utekelezaji. Hii mikataba ndiyo itakayosema sasa mradi wetu utakuwa namna gani, tunashirikiana kwenye eneo gani na mikataba hii itakuwa mingi, hautakuwa mmoja.
“Kama ni mkataba wa mifumo bandarini, ushushaji na upakuaji wa mizigo; kama ni mikataba ya kujenga maeneo ya kuhifadhi, kwa kadiri tutakavyokubaliana tutakuja kuwajulisha,” aliongeza Msigwa.
Upokeaji maoni unaendele
Hata hivyo, alisema bado wanasikiliza maoni ya wananchi kupitia njia mbalimbali.
“Kwa hiyo wadau wakizungumza, Serikali tunapokea hayo maoni tunazingatia na wawekezaji tutakaoshirikiana nao. Majadiliano ni pamoja na kupokea maoni,” alisema Msigwa, huku akisisitiza kuwa bandari haijauzwa.
“Mpaka sasa hakuna mradi wowote wa utekelezaji tuliosaini, tulichosaini ni makubaliano ya ushirikiano ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Dubai kwamba tutashirikiana kwenye uendelezaji wa bandari. Tunaendeleza wapi, kwa kiasi gani, kwa muda gani, itakuwamo kwenye mradi.”

Comments
Post a Comment